Dodoma. Watumishi saba wa Serikali wamefariki dunia na wengine watatu kujeruhiwa baada ya magari waliyokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso katika kijiji cha Mbande, kata ya Sejeli wilayani Kongwa jijini Dodoma.
Ajali hiyo imetokea leo Jumamosi Novemba 3, 2018 saa 6 usiku ikihusisha gari la Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Murotto amesema gari STL 6250 Toyota Land Cruiser mali ya ofisi ya CAG iliyokuwa ikiendeshwa na Dickson Kitanda (42) mkazi Dar es Salaam ikitokea Dodoma kwenda Dar es Salaam ikiwa na abiria sita ililigonga kwa nyuma lori lililokuwa limeegeshwa pembeni ya barabara.
Amesema baada ya kugonga lori hilo, gari hilo lilihamia upande wa pili wa barabara na kugongana uso kwa uso na gari nyingine SU 41173 Toyota Land Cruiser GX mali ya PSSSF iliyokuwa ikitokea Dar es Salaam kuelekea Dodoma.
Amesema gari ya PSSSF ilikuwa ikiendeshwa na Peter Eleson (35) mkazi wa Dodoma ilikuwa na abiria watatu; Eliad Eliyakunda Mdeme (40) ambaye ni mwanasheria, Vick Elisala Moshi (51), Katibu muhtasi wa mkurugenzi mkuu wa PSSSF na Abubakar Mjata Ndwaqta (42) ofisa takwimu wa PSSSF.
Amesema miili ya marehemu imepelekwa hospitali ya Kongwa na majeruhi watatu wamelazwa Hospitali ya Rufaa mkoa wa Dodoma .