Serengeti. Polisi Wilayani Serengeti Mkoani Mara Tanzania, inawashikilia mume na mke kwa tuhuma za kumkeketa binti yao wa miaka 14 kinyume cha sheria.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Daniel Shillah amesema hayo leo Jumapili Aprili 12, 2020 kukamatwa kwa mume huyo mwenye umri wa miaka 64 na mkewe (50), wote wakazi wa Kijiji cha Kitarungu Kata ya Nyansurura.
Amesema wanandoa hao walitiwa mbaroni Aprili 11, Saa 7 usiku nyumbani kwao muda mfupi baada ya kutekeleza ukatili huo.
Mganga Mkuu wa Hospitali Teule ya Nyerere, Tanu Warioba jana Jumamosi Aprili 11 alipozungumza na Mwananchi, alisema alimpokea binti huyo ambaye ni mwanafunzi wa darasa la sita akiwa amekeketwa.
“Ni kweli amekeketwa na akafikia hatua ya kuvuja damu nyingi ameletwa akiwa hajiwezi tumemlaza kwa ajili ya matibabu,” amesema.
Mkurugenzi wa Kituo cha Matumaini kwa watoto wa kike na wanawake Tanzania, Rhobi Samwel akizungumza na Mwananchi, amesema walipata taarifa kwa wasiri wao kuhusu ukeketaji unaofanywa hivi sasa nyumba kwa nyumba usiku, na kutoa taarifa dawati la jinsia la polisi na kufanikiwa kuwaokoa mabinti wawili kati ya watatu waliotakiwa kukeketwa.
Pia Soma
- Nec kutumia Sh180 bilioni uchaguzi mkuu
- ANTI BETTIE: Natamani aniache, harufu ya pombe anazokunywa inanishinda
- TUONGEE KIUME: Kukosa kazi kunachangia kuharibu mahusiano
Hilo ni tukio la pili la watu kukamatwa kwa tuhuma za kuwakeketa watoto wa kike katika kipindi hiki cha likizo ya corona.