Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Watuhumiwa 70 wa uhalifu wakamatwa Shinyanga

Kamanda Msa Shy4 01 24 At 15.jpeg Watuhumiwa 70 wa uhalifu wakamatwa Shinyanga

Wed, 24 Jan 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Miongoni mwa majukumu ya Jeshi la Polisi Tanzania ni pamoja na kubaini wahalifu na kuzuia uhalifu, Jukumu hili linaelezwa kufanywa vizuri na Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga likiongozwa na Kamanda ACP Janeth Magomi ambaye katika kuimarisha ulinzi na usalama akiwa na kikosi cha askari polisi mahiri ameendelea kufanya doria na misako mbalimbali ili kubaini na kuzuia kuhalifu ambapo wamefanikiwa kukamata watuhumiwa pamoja na vielelezo mbalimbali.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Jumatano Januari 24, 2024, Kamanda Magomi amesema katika doria na misako waliyoifanya kati ya Disemba 21, 2023 hadi Januari 23, 2024 wamefanikiwa kukamata mali mbalimbali pamoja na watuhumiwa 76 ambao walikamatwa katika vituo mbalimbali.

"Tumefanikiwa kukamata bunduki 01 aina ya Shortgun Pump Action yenye namba za usajili MV. 95738V ambayo iliibiwa huko katika kijiji cha Mondo Wilaya ya Kishapu Mkoa wa Shinyanga, pia tumekamata simu 02, mafuta ya dizeli lita 100, pikipiki 08, Betri 03 za gari, Kompyuta mpakato (Laptop) 02, EMS Foot massager 01, Redio 01 na spika 01," amesema Kamanda Magomi.

Amevitaja Vitu vingine vilivyokamatwa ni pamoja na vipande 120 vya nondo, mifuko 04 ya unga wa ngano, mafuta ya kula lita 15, Vipande 08 vya bomba, vipande 09 vya vyuma (angle line), Mashine 02 za kusukuma maji, Extension cable 01, Grander 01, Sigara pakiti 30, Pombe ya moshi lita 105, Mirungi bunda 94, Boksi 05 za vifaa tiba aina ya Gloves, Goroli 125 za kusaga mawe, mapipa 04, sufuria 01, bhangi kilo 02 na kete 10 pamoja na vifaa mbalimbali vya kupigia ramli chonganishi.

Kwa upande wa kesi Mahakamani, jumla ya kesi 11 zimepata mafanikio ambapo kesi 02 za kubaka washtakiwa 02 walihukumiwa miaka 30 jela, kesi 01 ya wizi wa mifugo washtakiwa 02 walihukumiwa miaka 02 jela, kesi 01 ya kujeruhi mshtakiwa 01 alihukumiwa mwaka 01 kifungo cha nje, kesi 01 ya wizi mshtakiwa alihukumiwa miezi 09 jela, shambulio la kudhuru mwili kesi 03 washtakiwa 03 walihukumiwa miezi 03 jela, shambulio la kawaida kesi 02 washtakiwa 02 walihukumiwa kwenda jela kati ya miezi 03 hadi 06 na kuingia kwa jinai kesi 01 mshtakiwa alihukumiwa kwenda jela miezi 03.

"Katika kuhakikisha ajali za barabarani zinadhibitiwa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga kitengo cha Usalama Barabarani limefanikiwa kukamata jumla ya makosa 4846 ambapo makosa 4844 watuhumiwa waliwajibishwa kwa kulipa faini za papo kwa papo, makosa 02 yaliyohusisha ajali kwa kukiuka taratibu,kanuni na Sheria za Usalama Barabarani yalifikishwa Mahakamani na washtakiwa kulipa faini za Mahakama na kuonywa kutorudia makosa," ameongeza Kamanda Magomi.

Katika hatua nyingine amesema Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linawashukuru wananchi kwa kuendelea kutoa ushirikiano katika kupambana na uhalifu na wahalifu kwa kutoa taarifa. Sambamba na hilo linawataka madereva na watembea kwa miguu kutii na kuheshimu alama, michoro na Sheria za Usalama Barabarani wakati wote wanapokuwa barabarani.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live