Akizungumza na waandishi wa habari jijini Mwanza jana Mongella ametaja kundi jingine linaloshauriwa kufuatilia shughuli hiyo kupitia vyombo vya habari ni pamoja na wazee na wale wenye maradhi.
“Maandalizi yote kwa ajili ya heshima za mwisho kwa Hayati John Magufuli katika viwanja vya CCM Kirumba yamekamilika. Hata hivyo, tunawasihi wazazi na walezi kuzuia watoto wadogo kuhudhuria shughuli hiyo kuepuka madhara ya msongamano. Wazee na wenye maradhi mbalimbali pia tunawashauri kufuatilia tukio hilo kupitia luninga,” amesema Mongella.
Mkuu huyo wa mkoa amesema milango yote ya uwanja wa CCM Kirumba itakuwa wazi kuanzia saa 12 asubuhi kwa ajili ya waombolezaji kuingia kwa ajili ya kutoa heshima za mwisho.
Kesho Jumatano Machi 24, 2021 wakazi wa Mwanza nao watapata fursa ya kumuaga kiongozi huyo atakayezikwa wilayani Chato Mkoa wa Geita Ijumaa Machi 26, 2021.