Tabora. Watumishi mkoani Tabora, wameonywa juu ya kutoa siri za vikao vya kiutendaji kwa viongozi wa kisiasa.
Imeelezwa kwa kufanya hivyo, wanaweza kusababisha msuguano usio na sababu kati ya viongozi wa kiserikali na viongozi wa kisiasa.
Akizungumza katika kikao cha tathmini ya watendaji kilichofanyika leo Ijumaa Julai 5, 2019, Kaimu Katibu tawala wa mkoa wa Singida, Tanzania, Natalis Linuma amesema wapo baadhi ya watendaji, wenye tabia za kupenyeza mambo kwa madiwani na kuleta mtafaruku kwenye vikao vinavyohudhuriwa na madiwani hao.
Amewataka kutumia utaratibu uliowekwa ambao ni pamoja na kumweleza Mkurugenzi mtendaji ambaye atajua namna ya kulishughulikia.
Amewataka watumishi kuwaheshimu viongozi wa kisiasa na kushirikiana nao ingawa ameweka angalizo kuwa kila mtu ajue na kutekeleza wajibu wake pasipo kuingiliana.
Kikao hicho cha siku tano, kinachohitimishwa leo, kinahudhuriwa na watendaji mbalimbali wa ngazi ya kata na maofisa tarafa wa Wilaya ya Kaliua.