Mwanza. Viongozi wa Serikali za mitaa mkoa wa Mwanza hasa watendaji wa kata, vijiji na mitaa ndiyo vinara wa vitendo vya rushwa vilivyoripotiwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo, Mkuu wa Takukuru mkoa wa Mwanza, Ernest Makale alisema kati ya taarifa na malalamiko ya rushwa 80 yaliyopokelewa kati ya Julai hadi Septemba mwaka huu, 58 ziliwahusu watumishi hao.
Malalamiko 24 yaliwahusu watendaji wa kata, vijiji na mitaa, wakati idara za elimu na ardhi zikifuatia kwa kuwa na malalamiko 12 kila idara.
Idara nyingine na idadi ya malalamiko kwenye mabano ni afya (5), uvuvi (4), wakati kilimo na mifugo zikilalamikiwa mara moja.
“Taasisi nyingine zilizolalamikiwa ni Mahakama yenye malalamiko tisa, Jeshi la Polisi mara nne, ujenzi malalamiko matatu huku vyama vya siasa tukipokea malalamiko mawili. Serikali Kuu moja, nishati na vyombo vya habari tumepokea lalamiko moja kwa kila taasisi,” alisema Makale.