Mbozi: Zaidi ya Sh260milioni za makusanyo katika halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe zinadaiwa kutafunwa na baadhi ya watendaji wa halmashauri hiyo.
Akizungumza leo Alhamisi Mei 30, 2019 katika kikao cha watendaji hao mwenyekiti wa halmashauri ya Mbozi, Erick Ambakisye amedai watendaji hao wameingia katika mtego na kupoteza uaminifu kwa kutumia fedha za umma kinyume na taratibu.
“Ninawaonya ambao hawajawasilisha fedha wafanye haraka kabla ya Juni 6, 2019 vinginevyo hatua kali zitachukuliwa,” amesema Ambakisye.
Amesema wakati fedha hizo zikitafunwa wamegundua akaunti feki ya mashine za kielektroniki inayotumika kuchepusha mapato ya halmashauri, akibainisha kuwa zaidi ya Sh80milioni zimeingizwa katika akaunti hiyo.