Mkurungenzi wa Jiji la Tanga, Said Majaliwa amewataka maofisa mapato kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato, ikiwemo kuweka vizuizi vya ukaguzi kwenye mipaka yote, ili kuhakikisha kila chanzo kinakusanywa bila ya kuruhusu uchepushaji.
Hayo ameyasema wakati wa kikao chake na timu ya ukusanyaji wa mapato, ili kuweka mipango ya kufikia lengo la ukusanyaji la Sh bil 19 kwa mwaka 2023/24.
Ameitaka timu hiyo kutokukaa ofisini, badala yake watoke kwenda kukusanya mapato kwa kushirikiana na viongozi wa kata na mitaa kwenye maeneo yao.
"Sitavumilia uzembe katika ukusanyaji wa mapato na kusababisha upotevu, lazima kila chanzo cha mapato mkibaini na muhakikishe mnakusanya mapato hayo, "amesema Mkurungenzi Majaliwa.
Amewaasa kufanya kazi ya ukusanyaji wa mapato bila ya vurugu au mabavu, ili zoezi hili lisiweze kuwa kero kwa wananchi.