Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri amewataka wananchi waliopitiwa na barabara ya njia nne watakaolipwa fidia kuzitumia fedha watakazopata kuwekeza kwenye shughuli mbalimbali ikiwemo kilimo na ufugaji ili kujiongezea kipato.
Shekimweri aliyasema hayo wakati akizungumza na wakazi wa Mtaa wa Vikonje na Mtumba, Kata ya Mtumba.
Alisema kutokana na ujenzi wa barabara ya njia nne baadhi ya wananchi watalipwa fidia ili kupisha ujenzi wa miundombinu hiyo hivyo ni vyema wakatumia fedha hizo kwa ajili ya kuwekeza kwa ajili ya maendeleo yao.
"Mtakaolipwa fedha kwa ajili ya fidia ni vyema mkawekeza katika kilimo cha zao la zabibu, ufugaji na uvuvi, badala ya kuzielekeza kwenye anasa zisizo na tija," alisema.
Aidha, Shekimweri aliwataka wananchi hao kuzitumia fedha hizo pia kwa kununua ardhi nyingine watakayoitumia kwa matumizi mbalimbali, kununua chakula cha kutosha kwa ajili ya kujihami na njaa pamoja na kuwekeza kwenye suala la elimu kwa watoto.
"Mfano wanapewa milioni 40 hapa kama ni wazee watu wazima awe mwanaume au mwanamke lazima atageuka kuwa kijana mwenye miaka 19 na atatafuta dogodogo na kusahau kuwa fedha hizo zinatakiwa kuwekezwa kwenye miradi mbalimbali ya kimaendeleo. Naomba niwasisitizie mkafanye matumizi sahihi," alisema.
Mkazi wa Vikonje, John Petro alisema wananchi wanatakiwa kupewa elimu kabla ya kulipwa fidia ili fedha hizo zitumike kwa manufaa na maendeleo yao.