Arusha. Naibu Waziri wa Kilimo, Omary Mgumba amesema Serikali inatambua umuhimu wa kuwajengea uwezo wadau mbalimbali wa kutumia ipasavyo viuatilifu vya wadudu kuhakikisha visumbufu haviwi kikwazo katika kutimiza azma ya serikali ya kufikia uchumi wa kati ifikapo 2025.
Mgumba ametoa kauli hiyo leo Jumanne, Mei 28, 2019, alipokuwa akifungua kongamano la siku nne la kimataifa la kisayansi kuhusu matumizi na athari za viuatilifu kwa afya ya binadamu na mazingira, kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara linalofanyika katika Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu Tanzania (TPRI).
“Kongamano hili litakuwa jukwaa zuri la kujifunza na kubadilishana uzoefu na utaalamu pamoja na sera za mbinu bora za matumizi sahihi ya viuatilifu katika kudhibiti visumbufu kwa nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara.
“Pia, kushughulikia changamoto mbalimbali za kikanda na kimataifa zinazotokana na matumizi yake,” amesema Mgumba.
Amesema licha ya changamoto hizo, lakini viuatilifu vina umuhimu wake katika kuzalisha mazao.
Amesema inaelezwa kuwa visumbufu vya mazao, husababisha upotevu wa karibu nusu ya mazao barani Afrika na kama Afrika inakusudia kuzalisha chakula cha kutosha kwaajili ya watu wake, wakulima hawana budi kupambana navyo.
Pia Soma
- Apoteza maisha ndani ya ndege
- Utouh ‘alibip’ Bunge, adai halisimamii mapendekezo ya CAG
- Magufuli atua Zimbabwe
Amesema kupitia ubalozi huo, wanatoa ufadhili wa masomo ya elimu ya juu yanayohusu kilimo katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na Udhamivu nchini Ufaransa kwa lengo la kuinua sekta hiyo nchini.
Kaimu Mkurugenzi wa TPRI, Dk Margaret Mollel amesema upo umuhimu wa kuunganisha nguvu za pamoja katika kuhakikisha kuna matumizi mazuri ya viuatilifu bila kuathiri afya za binadamu na mazingira.