Dodoma. Mkurugenzi wa jiji la Dodoma, Godwin Kunambi amesema jiji halitosita kumnyima kibali mtu yeyote atakayekiuka agizo la kupanda mti kwenye eneo la kiwanja chake
Mkurugenzi Kunambi ameyasema hayo leo jijini hapa wakati wa kuingia makubaliano baina ya jiji na Wakala wa Huduma ya Misitu Tanzania (TFS) wa kupanda miti ya kivuli milioni 15 kwa kipindi cha miaka mitano.
Lengo la makubaliano hayo ni ili kuboresha mazingira kwa kulifanya Jiji la Dodoma kuwa kijani na kuwa mfano katika maeneo mengine.
Amesema ili lengo hilo lifanikiwe kwa kiwango kinachotakiwa ni lazima kila mwenye kiwanja aanze kupanda miti ya kivuli na matunda kabla hajaanza kujenga.
"Yeyote anayetaka kujenga lazima aanze kupanda miti katika eneo lake, hivyo anayekuja kwetu na ramani yake ili tumpatie kibali sisi kama jiji la Dodoma hatutaona haya kukataa kutoa kibali kama hatatuonyesha miti aliyopanda," amesema Kunambi.