Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara- Mikindani, imeeleza kusikitishwa na hujuma, zinazofanywa na baadhi ya wananchi, kwa kung’oa vibao vya anuani ya makazi ,
Kufuatia hatua hiyo, Halmashauri hiyo kwa kushirikiana na vyombo vya dola, inatarajia kuanzisha msako mkali, kwa ajili ya kuwakamata watu wote wanaofanya hujuma hizo.
Akizungumza na Habarileo online Mkurugenzi wa Manispaa ya Mtwara -Mikindani, Kanali Emmanuel Mwaigobeko, amesema halmashauri imewaomba wananchi kuwa walinzi na kutoa taarifa kwa vyombo vya sheria kuhusu wanaojihusisha na ung'oaji wa vibao vya anuani za makazi.
"Tunarajia kufanya msako ili kuwabaini na kuwachukulia hatua watakaobainika kujihusisha na ung'oaji wa vibao vya anuani za makazi na kuwachukulia hatua za kisheria, ikiwa ni pamoja na kurejesha gharama zote ambazo zilihusika kuweka hizo anunani," amesema
Mwenyekiti wa mtaa wa Mtepwezi Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Hashimu Mbutuka amekiri kuwepo kwa wimbi la wizi wa vibao hivyo katika mtaa wake, na kwamba tayari vibao sita vimeng’olewa.