Tabora. Baadhi ya wakazi wa kijiji cha Igungwa wilayani Sikonge Mkoa wa Tabora wamesema ndege iliyoanguka na kuua watu wawili ilianza kuzunguka hewani bila mwelekeo.
Wakizungumza na Mwananchi leo Jumapili Agosti 4, 2019 wamesema baada ya hali hiyo walisikia kishindo, walipokimbilia eneo ilipoanguka walikuta ikiwaka moto.
Ndege hiyo yenye usajili ZU-TAF aina ya SLG4 ilianguka jana wakati ikiruka kutoka kiwanja cha ndege cha Tabora kuelekea kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Lilongwe, Malawi ikiwa na abiria wawili raia wa Afrika waliopoteza maisha, Desmond Roy Werner (rubani) na Werner Froneman (mhudumu).
Itobelo Nhungami amesema alishuhudia ndege hiyo ikizunguka hewani huku ikienda kushoto na kulia na kisha kuanguka.
"Ilikuwa kazi ngumu kusogelea mahali ndege ilipo na kukata miti kuokoa miili ya watu waliokuwemo,” amesema mkazi wa kijiji hicho, Mkambozi Kasembo.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya ya Sikonge, Peres Magiri amesema ndege hiyo ilikuwa ikienda nchini Malawi ikitokea mjini Tabora.
Habari zinazohusiana na hii
Amebainisha kuwa eneo ambalo ndege hiyo imeanguka litalindwa hadi wataalamu wa mambo ya anga watakapowasili kwa ajili ya kufanya uchunguzi, kwamba miili imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora ya Kitete.Amebainisha kuwa ndege hiyo ilikuwa mali ya shirika moja la Afrika Kusini, imetengenezwa nchini Urusi.