Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wapongezwa kusimamia vyema ujenzi wa hospitali

D73ae4a34032bd446415571b81d6db86.jpeg Wapongezwa kusimamia vyema ujenzi wa hospitali

Sat, 24 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MKUU wa Mkoa wa Katavi, Juma Homera, ameupongeza Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kwa kusimamia vizuri ujenzi wa Hospitali ya Wilaya unaoendelea katika eneo la Isinde, Kata ya Mtapenda.

Homera alitoa pongezi hizo jana katika ziara yake ya kukagua na kuhimiza shughuli mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na wananchi kwa kushirikiana na serikali ikiwemo ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nsimbo.

Pamoja na pongezi hizo, aliwataka mafundi wazawa wanaotekeleza ujenzi huo kuongeza kasi ya ujenzi ili kuhakikisha hospitali hiyo inakamilika kwa wakati ili wananchi wa Nsimbo waweze kunufaika na huduma bora za afya.

Alisisitiza kuwa umakini katika usimamizi wa rasilimali za ujenzi zilizonunuliwa zinazotumika katika ujenzi huo ili hospitali hiyo iwe na ubora na viwango vinavyotakiwa.

Mhandisi wa ujenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo, Martin Felician alisema mpaka sasa, Sh milioni 300 zimetumika katika ujenzi wa majengo yote kati ya Sh milioni 500 zilizokwishapokewa.

Felician alisema mpaka sasa majengo yaliyojengwa kwa fedha iliyopokewa ni pamoja na jengo la wagonjwa wa nje (OPD), jengo la maabara pamoja na jengo la kuchoma taka, yote yako katika hatua ya kuanza kupauliwa kwa ajili ya kuezekwa.

Aliongeza kuwa wanatarajia kupokea Sh bilioni 1 ili kuendeleza ujenzi huo ambapo amemhakikishia mkuu wa mkoa kuwa mara fedha hizo zitakapofika, ujenzi huo utakamilika kwa wakati kwa kuzingatia ubora na viwango vinavyotakiwa.

Chanzo: habarileo.co.tz