Dar es Salaam. Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Handeni Mkoani Tanga, Athman Malunda amewataka wanaume wakware kuwashonea wake zao sare za shule ili wasiendelee kuwatamani wanafunzi wa kike na kuwasababishia mimba.
Akizungumza katika maadhimisho ya Juma la Elimu lililoandaliwa na Mtandao wa Elimu (TENMET) Wilayani Handeni leo Mei 30,2019 Malunda amesema ili kudhibiti tatizo la mimba shuleni lazima wanaume wenye tabia ya kujihusisha kimapenzi na wanafunzi wadhibitiwe.
"Ukiona unamtamani mwanafunzi nenda kamshonee mkeo sketi mnunulie shati na begi akivaa basi atapendeza na utaacha kufuata fuata wanafunzi," amesema Malunda.
Awali Naibu Katibu Mkuu wa Tamisemi anayeshughulikia elimu Tixon Nzunda aliwataka wanafunzi wa kike kujitambua ili waweze kutimiza ndoto zao.
"Jueni kwamba hiyo miili yenu ina thamani kubwa kwa hiyo msikubali aishike na mkiona kuna mtu anataka kufanya hivyo nendeni mkaseme kwa walimu au wazazi," amesema Nzunda.
Amesema Serikali imeandaa mikakati ya kuhakikisha wanafunzi wote wanaoanza darasa la kwanza wanamaliza shule bila kuwapo kuishia njiani.
Pia Soma
- VIDEO: Serikali yamkana Hapi kuhusu vitambulisho
- Uhaba wa walimu kukwamisha ndoto ya Handeni kuwa kinara kwenye elimu
- Kilo 400 za nyama zilizoharibika zateketezwa Arusha
Mwakilishi wa TENMET na Mkurugenzi wa Hakielimu Dk John Kalage amesema mafanikio ya Juma la Elimu ambalo huwa linafanyika kila mwaka kwenye wilaya mbalimbali ni kuongezeka kwa ufaulu kutokana na changamoto zinazojitokeza kushughulikiwa.