Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanaotorosha mifugo nje ya nchi kushtakiwa kwa uhujumu uchumi

79876 Waziri+pic

Tue, 15 Oct 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Arusha. Naibu Waziri Wizara ya Mifugo na Uvuvi wa Tanzania, Abdalah Ulega  amewaonya wafugaji wenye tabia ya  kutorosha mifugo na kuipeleka nje ya nchi kuacha mara na atakayekamatwa, atashtakiwa kwa makosa ya uhujumu uchumi.

Ameyasema hayo leo Jumapili Oktoba 13, 2019 wakati akizungumza katika ufungaji wa semina ya  uuzaji wa ng'ombe kwa kutumia mizani, iliyowashirikisha wafanyabiashara , wafugaji na wenyeviti wa vijiji. Semina hiyo imefanyika katika mpaka wa Namanga.

Ulega amesema wafugaji wengi wana tabia  ya kutorosha mifugo nje ya nchi kwa kisingizio cha soko.

Amewataka kuuza  mifugo hiyo nchini kwa sababu hivi sasa mifugo yote inapimwa kwa kilo, haikadiriwi kama ilivyokuwa awali.

Amesema wafugaji wengi hupeleka mifugo yao nje ya nchi kutokana na uhakika wa soko  kwa madai kuwa huko hununuliwa  kwa kilo badala ya kukadiria.

“Mfugaji  yeyote atakayepatikana akisafirisha  mifugo nje ya nchi  atashtakiwa kwa kosa la uhujumu uchumi na atapelekwa jela na  hatajua atatoka lini, hivyo nawaomba mfuate sheria na taratibu za nchi,” amesema Ulega.

Pia Soma

Advertisement
Akizungumza katika ufungaji huo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Longido, Jumaa Mhina amesema katika kudhibiti utoroshaji wa mifugo unaofanywa na baadhi ya wafugaji, tayari wamejenga mnada mkubwa wa kisasa  wilayani Longido ambao umeanza kutumiwa na wafanyabiashara na wafugaji.

 

Amesema uwapo wa mnada huo utawezesha wafugaji kupeleka mifugo yao ambayo itakuwa ikipimwa kwa kilo badala ya kukadiria  na tayari mizani zimeshaletwa kwenye eneo hilo.

“Kwa kufanya hivi, wafugaji sasa watanufaika kwa kuuza bei halisi na halali itakayowapatia faida,” amesema mkurugenzi huyo.

Mhina amesema mnada huo unapokea ng'ombe 300 kwa siku na mbuzi  2,000, na  biashara ya kununua na kuuza mifugo katika eneo hilo tayari ilishaanza.

Amesema changamoto bado ipo kwenye elimu jinsi ya kutumia mizani  hiyo kwa wafugaji na wafanyabiashara ambayo amesema inaendelea kutolewa.

Mmoja wa wafugaji, Olesiada Sadala amesema semina hiyo imewasaidia kujua matumizi sahihi ya mizani na umuhimu wa kufuata sheria na kanuni kama kulipa kodi.

Amesema kuanzishwa kwa mnada huo wa mifugo pia kutasaidia kuondosha tatizo la   kutorosha mifugo.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz