Mwanza. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linawashikilia watu 18 kwa tuhuma za wizi wa pikipiki.
Mbali na kukamatwa kwa watu hao, polisi pia limekamata pikipiki 16 zilizokuwa zikitumika katika wizi huo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano Julai 31, 2019 Kamanda wa polisi mkoani Mwanza, Jumanne Muliro amesema matukio hayo yametokea kati ya Januari hadi Desemba 2018, na Januari hadi Julai, 2019.
“Mafanikio ya kuwakamata wahalifu hao wakiwa na vielelezo vya pikipiki zilizoporwa yametokana na ushirikiano wa vikosi mbalimbali vya polisi vilivyopo katika mikoa ya Mwanza, Mara katika wilaya za Tarime na Rorya,” amesema.
Kwa mujibu wa Muliro kazi ya ufuatiliaji imefanyika baada ya kubaini kuwepo kwa ongezeko la unyang'anyi wa pikipiki na baadhi ya vijana kujeruhiwa na wengine kufariki dunia kati ya mwaka jana na mwaka huu.
Aliyataja maeneo yaliyoathirika ni Nyakabungo, Nyakato, Buhongwa, Isamilo, Ibanda, Kiseke, Kishiri, Maduka tisa, Nyamhongoro, Ngudu wilaya ya Kwimba na Sengerema.
Pia Soma
- Diwani ahoji kata kuitwa Zuzu, ataka iitwe Zinje
- Madiwani Mbozi wataka muda zaidi usajili laini za simu
- Kaulia waanzisha mfuko wa elimu
Muliro amesema wanakamilisha taratibu ili watuhumiwa hao wafikishwe mahakamani.
Katika tukio lingine, polisi wamefanikiwa kuwakamata Frank Ayub (22) na Khalifa Mohamed (20) wakiwa wamevalia sare zinazofanana na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Amesema walikamatwa Julai 22, 2019 eneo la Bwiru wilayani Ilemela.