Serengeti. Wakazi wa kijiji cha Bisarara Wilaya ya Serengeti wamemuua kiboko aliyeingia katika kijiji hicho kutoka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na kumchinja kisha kugawana nyama.
Akizungumza leo Jumatatu Februari 3, 2020 mwenyekiti wa Serikali ya kijiji hicho, Thomas Marwa amesema mnyamapori huyo alionekana katika eneo la Kisangura ambalo wanafunzi huvuka kwenda upande wa pili.
Awali, wananchi waliona alama za miguu ya kiboko katika mashamba na kupeana taarifa na baada ya muda walimuona na kuanza kumshambulia kwa silaha mbalimbali.
“Ndani ya dakika kumi walikuwa wameishamuua na kugawana nyama, ilikuwa shangwe maana walikamilisha mwisho wa wiki vizuri. Nilikuta wameshagawana nyama, nilitoa taarifa kwa ofisa wa wanyamapori wa wilaya,” amesema.
Amesema mwaka 2019 viboko watatu waliuawa baada ya kuingia katika kijiji hicho.
Ofisa wanyamapori Wilaya ya Serengeti, John Lendoyani amekiri kupata taarifa ya tukio hilo na kuahidi kufuatilia.