Hai. Wananchi wa kijiji cha Mkalama wilayani Hai Mkoa wa Kilimanjaro wamemtaka mkuu wa Wilaya hiyo, Lengai Ole Sabaya kumwondoa mwekezaji katika shamba la Kikuletwa kwa madai kuwa amesababisha mgogoro.
Wakizungumza na mkuu huyo wa wilaya leo Alhamisi Novemba 22, 2018 wananchi hao wamesema mwekezaji huyo amewakodisha wananchi mashamba ekari moja kwa Sh400,000.
Wakizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo, Ibrahim Lugoma amemuomba Sabaya kuangalia namna ya ardhi yao kurudi mikononi mwao kwani wamechoshwa na mwekezaji huyo.
“Ardhi hii imeanza kutumiwa na wawekezaji na vijana wetu hawana pakwenda kwa hiyo tunaomba Serikali iangalie malalamiko yetu . Wawekezaji hawa tumewachoka maana hata maendeleo ya wananchi hawachangii,” amesema Lugoma.
“Tunaomba ardhi irudi mikononi mwetu. Kwanini hawa wawekezaji wateketeze familia zetu. Tunaomba ardhi yetu irudi hawa wawekezaji wamepokezana vya kutosha sasa hivi huyu ni wa 11.”
Marium Hussein ambaye pia ni mkazi wa kijiji hicho amesema wamekuwa wakinyanyaswa na mwekezaji huyo kwa kuwa ni wanyonge na hawathaminiwi na kudai kuwa mwekezaji huyo hatoi mashamba kwa wananchi zaidi ya matajiri wenzake.
Sada Urio amesema walikuwa wakitumia shamba hilo bila kuibuka migogoro lakini ilianza baada ya mwekezaji kuchukua shamba hilo.
Akizungumza baada ya kuwasikiliza wananchi hao Sabaya amempa siku saba mwekezaji huyo kumpa matumizi sahihi ya shamba hilo na kama ameshindwa kuliendesha alirudishe kwa wananchi hao.
Mwekezaji huo, Herman Twairu alipoulizwa kuhusu kukodisha wananchi shamba hilo kwa kiasi kikubwa cha fedha amesema hajawahi kulikodisha na kuhusu michango, amesema kwa miaka miwili alichangia Sh200milioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo.