Wananchi 42,542 kutoka katika wilaya sita zilizoko mkoani Kagera wameanza kuondokana na adha ya kukosa maji baada ya miradi saba inayotekelezwa kwa fedha za UVIKO 19 shilingi bilioni 4.8 kuanza kutoa huduma hiyo
Kaimu meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini -RUWASA - mkoa wa Kagera mhandisi Patrice Jerome amesema kuwa miradi yote saba imekamilika kwa kati ya asilimia 75 hadi 99 na kwamba baadhi yake imeanza kutoa maji
"Katika wilaya ya Muleba inatekelezwa katika majimbo mawili, la Kusini na Kaskazini, Bukoba upo wa Kashenge - Irogelo, upo wa Nkenge Missenyi, Buhenge - Kirusha wilaya ya Ngara, Nyakaiga Kakuraijo wilaya ya Karagwe na Murongo wilayani Kyerwa, tayari miradi sita imekwishaanza kutoa huduma, iko kwenye hatua ya uangalizi na majaribio," amesema mhandisi Jerome.
Baadhi ya wananchi waliozungumzia huduma hiyo wakiwamo wa mradi wa Kashenge - Irogelo ulioko kata Katoma katika wilaya ya Bukoba, wameishukuru serikali kuwapelekea mradi huo ambao umewaondolea tatizo la kutembea umbali mrefu kwenda mtoni.