Mradi huo ambao unagharimu shilingi bilioni 2.4 hadi sasa umekamilika kwa asilimia 95 na kwamba hadi kufikia mwanzoni mwa mwezi Julai utaanza kuwanufaisha wananchi.
Hayo yamebainishwa na Mhandisi msimamizi wa Mradi huo, James Ryoba wakati akizungumza na Waandishi wa Habari ambao walitembelea mradi huo, alisema mradi huo mkubwa wa maji una uwezo kuzalisha lita 240000 kwa saa.
Alisema mradi huo wa maji utaanza kutumika mwanzoni mwa mwezi Julai na kwamba zimebaki mita 700 kukamilika ili uanze kufanya kazi.
Alisema Mradi wa Ihumwa- Njedengwa ni miongoni mwa miradi mikubwa inayotekelezwa na Mamlaka ya majisafi na Usafi wa Mazingira mjini Dodoma (DUWASA) ili kuwafikia na kuwahudumia wakazi wote wa Dodoma.
“Jumla ya visima saba vinapeleka maji katika mradi huu zipo changamoto ambazo zilichelewesha kukamilika mapema kwa mradi ambapo kipande cha kilomita mbili kilichelewa kutokana na mradi kupita katikati makazi ya watu hivyo tulilazimika kuhamisha mabomba na kuyapeleka maeneo mengine ya wazi,” alisema Mhandisi Ryoba.
Katika hatua nyingine, Mhandisi wa usanifu na Ujenzi miundombinu ya maji taka, Aloyce Emirani alisema kwa sasa wanakabiliwa na uhaba wa miundombinu ya maji taka ambapo ni asilimia 20 tu ya mitambo ya maji waliyonayo.
Alisema kulingana na idadi ya watu ilivyo sasa ilitakiwa Jiji la Dodoma liwe na mifumo isiyopungua 10 ya mitandao ya maji taka ukilingalisha na sasa kuna mitambo minne yenye urefu wa mita 200 kwa 200.