Arusha. Katika kukabiliana na upungufu wa vyumba vya madarasa Mkoa wa Arusha umechukua hatua za dharura ikiwa ni pamoja na wanafunzi wa kidato cha kwanza kusoma kwa zamu wakati ujenzi wa madarasa ukiendelea
Hayo yameelezwa leo Jumapili Januari 6, 2019 na katibu tawala mkoa wa Arusha, Richard Kwitega katika mkutano wake na waandishi wa habari kuwaeleza hatua ambazo mkoa umechukua kuhakikisha wanafunzi wote wanaanza masomo kesho Jumatatu Januari 7, 2019.
“Nilikua na kikao kazi jana na wakurugenzi wote wa halmashauri za mkoa pamoja na wataalamu, tumeweka mikakati itakayowezesha wanafunzi wote kuanza masomo wakati madarasa yakikamilika ndani ya miezi mitatu,” amesema Kwitega
Amezitaja shule zitakazokuwa na utaratibu wa kusoma kwa zamu ni sekondari ya Akeri, Ngyeku, Mbuguni, Ngongongare na Nkoanrua zilizopo halmashauri ya wilaya ya Meru.
Nyingine ni shule za sekondari Kiranyi, Enyoito, Sokon II na Mukulat zilizopo halmashauri ya wilaya ya Arusha.
Nyingine ni sekondari ya Sombetini, Sinoni, Themi, Baraa, Kimaseki, Kinana, Ngarenaro, Olasiti na Suye zilizopo katika halmshauri ya jiji la Arusha.
Amesema wanafunzi 33,035 walifaulu ambayo ni sawa na asilimia 87 ya waliofanya mitihani ya kuhitimu darasa la saba na waliokuwa wamepata nafasi ya chaguo la kwanza ni 14,316 sawa na asilimia 43.