Dar es Salaam. Kikundi cha ngoma cha watoto kutoka Shule ya Fountain Gate Dodoma wanashiriki kwenye tamasha la ngoma za asili linalojulikana kama Tamasha la Utamaduni la Afrika Mashariki (Jamafest) jijini Dar es Salaam.
Tamasha hilo lililoanza juzi Jumamosi na kuzinduliwa jana Jumapili Septemba 22,2019 na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan linawakutanisha watu mbalimbali kutoka nchi sita za Afrika Mashariki na litamalizika Septemba 28, 2019.
Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa shule hiyo, Ahadi Mtweve amesema ushiriki wao umekuja baada ya kufanya vizuri kwenye tamasha la ngoma za asili lililofanyika wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma lililojulikana kama Cultural Music Festival (Cigogo) lililofanyika Julai 2019 na kuchaguliwa kuwa miongoni mwa vikundi vitakavyoiwakilisha Tanzania kwenye Jamafest.
“Tunathamini na kutoa kipaumbele kwa watoto wetu kushiriki michezo kama sehemu ya kukuza ufahamu wa kujifunza kwa ufasaha kupitia michezo.”
"Huwezi kumtenganisha mtoto na michezo, ukimpa mtoto nafasi ya kucheza atapenda shule na masomo pia” amesema Japhet Makau Mkurugenzi wa shule hiyo.
Makau amesema kwa nyakati tofauti wameshiriki matamasha mbalimbali ya kitaifa na kimataifa katika nchi za China, Ubelgiji, Norway na Afrika ya Kusini kama sehemu ya kuwafunza watoto kutambua fursa za michezo kama moja ya sekta muhimu inayotoa ajira.
Pia Soma
- Maiti yakaa mochwari kwa miaka 15 baada ya mke kugoma kumzika
- Anayepumulia mashine alazwa tena Mloganzila
- Mtoto wa mkuu wa majeshi Tanzania afariki ajali ya ndege