Jumla ya wanafunzi 76 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu katika shule tatu za sekondari zilizopo Urambo mkoani Tabora hawajaripoti shuleni.
Hayo yalibainishwa na Ofisa Elimu Sekondari wilayani humo, Philipo Balugahale, katika mkutano wa hadhara uliofanywa na Mbunge wa Urambo, Margaret Sitta uliofanyika katika kata tatu za mji mdogo wa Urambo Mchikichini, Kiyungi na Urambo.
Balugahale alisema hadi mwezi huu, jumla ya wanafunzi 76 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza hawajaripoti shuleni.
Alisema idara ya elimu ilifanya jitihada za kuitisha mikutano mbalimbali ya wazazi kuwataka wawapeleke watoto wao shuleni bila mafanikio.
Alitaja shule na idadi ya wanafunzi ambao hawajaripoti kwenye mabano ni Chetu (19), Ukombozi (45) na shule ya sekondari Urambo Day wanafunzi 12 hawajaripoti.
Alisema idara ya elimu ikifanikisha kuwapata wanafunzi hao watapelekwa shule bila masharti magumu kwa kupewa kibali maalumu.
Balugahale alisema takwimu hiyo ni ya wanafunzi wa shule za sekondari kwa kata tatu pekee kati ya kata 18 zilizopo wilayani humo.