Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanafunzi 11,200 kufanya mtihani darasa la saba Arusha, watamba kufanya vizuri

Mon, 9 Sep 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Arusha. Wanafunzi 11,200 katika halmashauri ya Jiji la Arusha nchini Tanzania wanatarajiwa kufanya mitihani ya kuhitimu elimu ya msingi itakayofanyika Jumatano na Alhamisi wiki hii.

Ofisa Elimu Msingi wa jiji hilo, Omari Kwesiga amesema hayo leo Jumatatu Septemba 9,2019 wakati akizungumza na Mwananchi juu ya maandalizi ya mitihani hiyo ambayo inahitimisha safari ya miaka saba ya wanafunzi hao.

Amesema kati ya wanafunzi hao wavulana ni 5,405 na wasichana ni 5,795 kutoka Shule 130 kati ya hizo shule za serikali ni 46 na binafsi ni 84.

“Tumejiandaa vizuri sana wanafunzi wetu wamefanya mitihani ya majaribio ya kutosha na jiji limefanya vizuri kwenye mtihani wa mwisho na kuziacha halmashauri zingine katika mkoa wetu kwa mbali, hivyo tunatarajia kufanya vizuri zaidi ya mwaka jana,” amesema Kwesiga

Kuhusu iwapo wamiliki wa shule binafsi kuwazuia wanafunzi wao kufanya mitihani kabla ya kumaliza ada na michango mingine amesema hakuna mwenye mamlaka ya kuwazuia wanafunzi kufanya mitihani kwa sababu ya kutokukamilisha ada au michango .

Amesema kama suala hilo lipo unapaswa kufanyika utaratibu kati ya mzazi na mmiliki wa shule namna ya kukamilisha malipo bila kumzuia mwanafunzi kufanya mitihani yake na kufanya hivyo ni kinyume cha Sheria.

Pia Soma

Advertisement
“Suala la kuwazuia wanafunzi katika Shule binafsi wasifanye mitihani kwa sababu za malipo mbalimbali halipo kabisa, naomba nitumie nafasi hii kuwatahadharisha wamiliki wa shule binafsi kufanya hivyo ni kinyume cha Sheria na ikitokea nitatoa taarifa kwa Kamishna wa Elimu aifutie hiyo Shule usajili,” amesema Kwesiga

 

Chanzo: mwananchi.co.tz