Moshi. Watu wawili waliofariki dunia wilayani Moshi, Mkoani Kilimanjaro kwa ugonjwa wa kimeta, wanadaiwa kula mzoga wa nyama ya ng'ombe ambaye alikua na vimelea vya ugonjwa huo.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Besti Magoma amesema leo Jumatano Februari 27,2019 kuwa wamelithibitisha hilo baada ya kuchukua sampuli ya nyama hiyo kwenda kuipima na kubaini uwapo wa ugonjwa huo.
"Tulichukua sampuli ya nyama iliyoliwa na watu hawa mnyama huyo alikuf ghafla na tumebaini ilikua na vimelea vya kimeta, hivyo tunaendelea kuwapa tahadhari watu kutokula nyama ambazo hazijapimwa na wataalamu,” amesema Dk Magoma.
Aidha, Magoma amesema hadi sasa ugonjwa huo umewakumba watu saba na tayari watu wawili wamefariki dunia na wengine wakiwa wamelazwa Hospitali ya KCMC.
“Hali za wagonjwa waliolazwa KCMC kwa kula nyama ambayo ilikua na vimelea vya kimeta wanaendelea vizuri na tayari tumeshatoa chanjo ya ugonjwa huo kwa watu 97,” amesema Magoma.