Morogoro. Mganga mkuu wa hospitali ya rufaa Mkoa wa Morogoro, Dk Ritha Lyamuya amesema waliofariki katika ajali ya moto mkoani humo wamefikia 94.
Amesema idadi hiyo imeongezeka baada ya majeruhi mmoja aliyekuwa amelazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kufariki dunia leo.
Hadi jana saa 10 jioni majeruhi wa ajali hiyo walifikia 21 kati ya 46 waliofikishwa Muhimbili kwa matibabu na vifo kufikia 93.
Ajali hiyo ilitokea Jumamosi iliyopita Agosti 10, 2019 katika mtaa wa Itingi, Msamvu barabara ya Morogoro-Dar es Salaam baada ya lori la mafuta kupinduka na kuwaka moto muda mfupi baada ya watu kuanza kuchota mafuta.
Lyamuya amesema mbali na vifo hivyo, majeruhi waliolazwa hospitali ya Morogoro wameongezeka kutoka 16 hadi 17 baada ya mmoja aliyekuwa ameruhusiwa nyumbani kurejea hospitali kutokana na kutojisikia vizuri.
Amesema mmoja kati ya majeruhi aliyekuwa katika hospitali hiyo amehamishiwa Muhimbili baada ya hali yake kubadilika.
Habari zinazohusiana na hii
- MAKALA YA MALOTO: Ukweli katili katika ajali lori la mafuta iliyotokea Msamvu
- VIDEO: RC Moro azungumzia hali za majeruhi ajali ya lori la mafuta
- Waliofariki ajali ya lori la mafuta Morogoro yafikia 75