WAZIRI wa Nishati January Makamba, amesema serikali imepanga kulipa fidia kwa wananchi 1,041 walioathirika na mradi wa umeme wa Rusumo ifikapo Septemba mwaka huu.
Makamba aliyasema hayo wakati akizungumza na wananchi wa eneo la Benaco lililopo wilayani Ngara, mkoani Kagera, ambapo amesema tayari tathmini iliyofanyika imebaini kuwa wananchi wanakidhi kulipwa fidia kutokana na madhara yaliyosababishwa na utekelezaji wa mradi huo unaohudumia nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi.
Alisema ulipaji fidia unaenda sambamba na ukarabati wa nyumba 304, ambazo zimepata madhara wakati wa utekelezaji wa mradi huo.
Alisema Wilaya ya Ngara itaondokana na changamoto ya umeme mdogo mara baada ya kukamilika mradi wa umeme wa Rusumo.
Awali Mbunge wa Ngara, Ndaisaba Ruholo, alisema kuwa mpaka sasa kwa kipindi cha miaka mine, wananchi hawajalipwa fidia na kumekuwa na uhakiki usiokuwa na mwisho, hivyo kumuomba Waziri suala la uhakiki lifikie mwisho ili wapate haki zao.