Mwanza. Jukwaa la walimu Wazalendo Halmashauri ya jiji la Mwanza nchini Tanzania limetoa mifuko 240 ya saruji kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Bulale.
Akizungumza wakati wa kukabidhi mifuko hiyo kwa mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Dk Philisi Nyimbi, katibu wa jukwaa hilo, Lucas Kondoko amesema wameguswa na adha wanayoipata wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata elimu.
“Tunaguswa sana kuona wanafunzi wanatembea umbali mrefu kufuata elimu, wakati mwingine mwanafunzi anafika shuleni ameshachoka hata akifundishwa anakuwa hazingatii masomo,” amesema Kondoko.
Amesema saruji hiyo yenye ya Sh4.2 milioni imepatikana baada ya kuchangishana ili kuwanusuru wanafunzi hao.
Dk Nyimbi amewapongeza walimu hao kwa hatua waliyoichukua na kuwataka watumishi wengine kuiga mfano huo, “itasaidia kuboresha elimu sio tu kwa wilaya hiyo pekee bali kitaifa.”
“Mmefanya kitu cha pekee mbali na changamoto kadhaa walizonazo lakini wameona wajinyime na kuwasaidia watoto wetu waweze kupata shule karibu na mazingira mazuri ya kusomea.”
Pia Soma
- VIDEO: Membe asema urais chanzo cha kufukuzwa uanachama CCM
- VIDEO: Ilichokisema Serikali ya Tanzania kuhusu virusi vya corona
- Mwenyekiti CCM alaani mauaji kiongozi wa Chadema
Kata ya Buhongwa yenye mitaa 18 ina wakazi 32, 000 ikiwa na shule za msingi tatu na sekondari moja ambayo licha ya kudaiwa kuzidiwa wingi wa wanafunzi lakini ipo mbali na wanafunzi hulazimika kutembea zaidi ya kilometa 10 kufuata.