Lindi. Tafiti zinaonyesha korosho ikivunwa ina uwezo wa kukaa zaidi ya mwaka mmoja bila kuharibika ikiwa itakaushwa na kutunzwa vizuri.
Zinaeleza kuwa ile dhana kuwa korosho ikivunwa baada ya miezi mitatu inaoza sio kweli.
Hayo yameelezwa leo Jumapili Agosti 4, 2019 na kaimu mkurugenzi wa kituo cha utafiti wa kilimo Naliendele, Dk Fortunatus Kapinga.
Amesema wana mifano ya korosho zilizovunwa mwaka 2017 na 2018 na bado zina ubora wake kutokana na utunzaji mzuri.
“Kinachosababisha korosho ikaoza baada ya kuvunwa kama mkulima asipoangalia, kama zitakuwa hazijakauka vizuri zinaweza zikaoza na hiyo sio kwa korosho pekee, hata mazao mengine ukiweka ghalani kama hayajakauka vizuri yataoza, lakini kama korosho itawekwa kwenye ghala lisilo na kiwango labda linavuja itaoza tu,” amesema Dk Kapinga.
Ameongeza, “Usiku wa baridi sana kuna unyevunyevu utajitokeza kwenye mabati utadondoshea matone kwenye korosho, na sisi tuna mfano wa korosho zilizozalishwa mwaka 2017 hadi leo ni nzuri na hata ukipeleka sokoni bado itanunuliwa.”
Pia Soma
- Siku nyeusi Marekani, wengine kumi wauawa kwa risasi Ohio
- Wanawake Chadema watakiwa kugombea uchaguzi Serikali za mitaa
- Alichokisema Dk Ndumbaro kuhusu maonyesho ya SADC
Mkulima wa korosho kutoka Nachingwea, Mariam Chilumba amesema mara kwa mara wamekuwa wakipewa elimu namna ya kulima zao hilo na kulihifadhi baada ya kuvunwa.