Dodoma. Serikali ya Tanzania itapeleka Sh115 milioni katika wilaya ya Karatu mkoani Arusha ili kuwasaidia wakulima wa vitunguu kupata visima, Bunge limeelezwa leo Alhamisi Juni 20,2019.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Kilimo Omary Mgumba ambaye ametaja fedha hizo zitapelekwa kwa mafungu mawili ikiwemo Sh40 milioni za Serikali na Sh75 milioni zitakazopitia mfuko wa TASAF.
Katika swali la msingi Mbunge wa Karatu (Chadema) Qambalo Willy Qulwi ameuliza Serikali ina mpango gani wa kuongeza vyanzo mbadala kama mabwawa na visima virefu ili kilimo katika bonde hili kiwe endelevu.
Naibu Waziri amesema vyanzo vya maji katika skimu za bonde la Eyasi ni mto Baray ambao hutiririsha maji kipindi cha masika pamoja na chemichemi ya Quangded ambayo hutiririsha maji kipindi chote cha mwaka.
Mgumba amesema serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya umwagiliaji katika bonde la Eyasi kulingana na upatikanaji wa fedha ambao uboreshaji huo utaokoa maji yanayopotea na hivyo kuyatumia katika uzalishaji.