Dar es Salaam. Mkurugenzi wa manispaa ya Kigamboni, Ng'wilabuzu Ludigija amewatahadhalisha wakazi wa manispaa hiyo kuhusu watu wanaojifanya maofisa wa Serikali wanaopita mitaani kukagua vibali vya ujenzi kisha kuwatoza fedha wananchi.
Ludigija ameeleza hayo leo Alhamisi Julai 4, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa utoaji wa vibali vya ujenzi unaofanywa na manispaa hiyo.
Amesema taarifa alizonazo, wanaojifanya maofisa wa Serikali na kuwatapeli wananchi wamewahi kuwa askari Mgambo wa manispaa ya Temeke.
Amesema wiki iliyopita mtu mmoja alikamatwa na watu hao kwa madai ya kutokuwa na kibali cha ujenzi na wakamuamuru kutoa chochote ili wamalizane na endapo akifikishwa katika ofisi za manispaa atatoa fedha zaidi kulingana na kosa hilo.
"Wamekuwa wakiamuru wananchi wasiokuwa na vibali vya ujenzi kutoa fedha kuanzia Sh150,000 hadi 300,000. Wakazi wa Kigamboni wasikubali kutoa fedha yoyote nje ya ofisi, malipo yote ya vibali yanafanyika katika ofisi za manispaa kwa mfumo rasmi,” amesema Ludigija.
Kuhusu utoaji wa vibali, mkurugenzi huyo amesema baadhi ya waombaji wanashindwa kukamilisha taratibu za kuomba ikiwemo kutolipa kodi ya ardhi hali inayosababisha wachelewe kupata vibali.