Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amezindua siku tano za maadhimisho ya wiki ya sheria na kuwataka wananchi kufika viwanja vya Mnazi Mmoja kupata msaada wa kisheria.
Akizungumza leo Jumamosi Februari Mosi, 2020 katika maadhimisho ya wiki ya sheria itakayohitimishwa na kilele cha siku ya sheria, Makonda amesema wananchi wenye matatizo ya kibiashara, migogoro ya ardhi na mirathi watasaidiwa.
Amesema katika maadhimisho hayo yanayofanyikwa viwanja vya Mnazi Mmoja kutakuwa na maofisa wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita), Jeshi la Polisi, Magereza na ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka (DPP).
"Wale waliokuwa wakija ofisini kwangu wanalalamika nawasihi waje katika viwanja vya mnazi mmoja ili mpate elimu haki zenu,” amesema Makonda.
Naye Jaji mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Lameck Mlacha amewataka wananchi kujitokeza kwenye viwanja hivyo kwa sababu watapokea kero zao na kuwapa msaada wa kisheria.