Wananchi wa kata ya Mlimani na Magadu manispaa ya Morogoro wameondokana na shida walizokuwa wakizipata kuvuka mto Kikundi kwenda upande wa pili baada ya ujenzi wa vivuko viwili uliogharimu Sh10.2 milioni kukamilika.
Kwa sasa wameondokana na usumbufu wa kusubiri saa moja hadi mbili ili maji yapungue waweze kuvuka nyakati za masika.
Diwani wa Magadu, Juma Kiduka amesema vivuko hivyo vimekamilika na vinaondoa adha hiyo iliyodumu kwa miaka 12.
Kiduka amesema vivuko hivyo vimejengwa kwa mataruma ya vipande vya reli baada ya wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (Sua) Morogoro kuomba vipande hivyo kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa aliyetoa mataruma ya reli 120.
“Wananchi wa kata ya Magadu, Mlimani na Luhongo wana kila sababu ya kuwapongeza wahadhiri wa Sua, Dk Abubakari Hoza, Profesa Romanus Ishongoma na wengine walioandika andiko la kuomba vipande vya mataruma ya reli kwa uongozi wa TRC,”amesema Kiduka.
Amesema kivuko cha kwanza kimejengwa kwa Sh7.5 milioni na kingine Sh2.7 milioni.
Advertisement Mkazi wa mtaa wa Nyandila kata ya Mlimani, Adrian Mkoba (40) amesema kabla ya ujenzi huo alikuwa akiwavusha wanafunzi, wanawake baada ya kushindwa kuvuka kwenda upande wa pili pale maji yanapokuwa mengi mtoni.
Kuna mwingiliano wa wakazi wa mitaa yetu inayotengenishwa na mto Kikundi na ilifikia wakati wanafunzi walikuwa wakishindwa kwenda shule kwa sababu mto umefurika maji hata watu wazima walikuwa wakisaidiwa kuvushwa kwa Sh5,00 hadi Sh1,000 kwa wenye mizigo,” amesema Elizabert Tanzania.