Ngara. Wafanyakazi wawili wa mradi wa maporomoko ya mto Rusumo wilayani Ngara mkoani Kagera wanahofiwa kufariki dunia baada ya gari lao kuacha njia na kupinduka leo.
Shuhuda wa ajali hiyo, Crispin Kamugisha ambaye pia ni mwenyekiti wa umoja wa wafanyabiashara wa mji mdogo wa Rusumo amesema pamoja na kuacha njia kutokana na kinachoaminika kuwa ni hitilafu kwenye mfumo wa breki, kupinduka kwa gari hilo pia kumesababishwa na ukungu uliotanda eneo hilo tangu alfajiri.
“Majeruhi wamekimbizwa hospitali ya Nyamiaga, haijajulikana mara moja idadi ya abiria waliokuwamo ndani ya gari hilo aina ya Toyota Coaster,” amesema Kamugisha.
Ajali hiyo imetokea wakati wafanyakazi hao wakienda kazini na tayari askari polisi wa usalama barabarani wamefika eneo la ajali.
Kamanda wa polisi mkoa wa Kagera, Revocatus Malimi amesema hajapata taarifa hizo na kuahidi kuzungumza baada ya kuwasiliana na watendaji wa polisi wilayani Ngara.
Endelea kufuatilia mitandao ya Mwananchi kwa taarifa zaidi.