Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wafanyakazi 50 Ngurdoto waachishwa kazi

C3d6edb17438b0b06aff81206e1a814b.jpeg Wafanyakazi 50 Ngurdoto waachishwa kazi

Mon, 10 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

UONGOZI wa Hoteli ya Kitalii ya Ngurdoto iliyopo nje kidogo ya Jiji la Arusha umewaachisha kazi wafanyakazi 50.

Wafanyakazi hao ni miongoni mwa watumishi 93 wa hoteli hiyo wanaodai malimbikizo ya mishahara Sh milioni 129.

Mei 3 mwaka huu Uongozi wa Hoteli uliwakabidhi wafanyakazi hao barua za kuwaachisha kazi kutokana na kinachodaiwa kuwa umekumbwa na changamoto za kibiashara.

Wafanyakazi hao waliogoma kuzipokea barua wakishinikiza kwanza walipwe fedha zao.

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Muro, alikwenda hotelini hapo kukutana na wafanyakazi akiwa amefuatana na maofisa kadhaa kutoka Idara ya Kazi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mfuko wa Hifadhi ya Jamii(NSSF) na watendaji wengine wa wilaya.

Muro alimtaka Mwanasheria wa Hoteli ya Ngrudoto, Edmund Ngemela, asitishe utoaji wa barua hizo ili waangalie namna sahihi ya kusuluhisha mgogoro baina ya wafanyakazi na mwajiri.

Ngemela alisema taratibu za kusitisha ajira za wafanyakazi 50 zilizingatiwa baada ya mteja wake (mwajiri) kuona kuna haja ya kufanya hivyo kutokana na mwenendo mbaya wa biashara uliomfanya ashindwe kumudu gharama za uendeshaji.

“Wafanyakazi walioachishwa kazi kutokana na changamoto za kibiashara watalipwa stahiki zao, isipokuwa walioacha wenyewe kwa kutofika kazini kwa mujibu wa sheria, ndio hawatalipwa,” alisema.

Meneja wa Hoteli ya Ngrudoto, Beatrice Dala’s, alisema waliamua kupunguza wafanyakazi kutokana na changamoto za kibiashara zinazotokana na ugonjwa wa Covid- 19 unaosababishwa na virusi vya corona.

Dala’s alisema walioachishwa wafanyakazi 50 wameachishwa kazi na wengine 13 wamejifukuza wenyewe kwa kutofika kazini kwa zaidi ya siku tano.

Mkurugenzi wa kampuni inayomiliki hoteli hiyo, Impala Group Limited, Joan Mrema, alisema mgogoro wa wafanyakazi na uamuzi wa Mahakama kuwa baadhi ya mali zao zikamatwe ni sehemu ya changamoto zilizosababisha washindwe kujiendesha biashara.

Joan alisema wafanyakazi wenye haki ya kulipwa stahiki zao watalipwa, hivyo wawe wavumilivu kwa kuwa kampuni ipo kwenye mipango itakayofanikisha malipo hayo.

Hivi karibuni Mahakama Kuu Kanda ya Arusha iliamuru baadhi ya mali za hoteli hiyo zikamatwe na zipigwe mnada ili kupata fedha za kulipa madai ya wafanyakazi 93 wanaodai malimbikizo ya mishahara sh milioni 129.

Chanzo: www.habarileo.co.tz