Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wafanyabiashara Ruvuma waeleza kero zao mbele ya mawaziri

77155 Songea+pic

Wed, 25 Sep 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Songea. Wafanyabiashara mkoani Ruvuma wametaja kero zao mbalimbali zinazosababisha washindwe kufanya biashara kama inavyotakiwa, kuiomba Serikali ya Tanzania kuzifanyia kazi.

Wameeleza hayo leo Jumanne Septemba 24, 2019 katika mkutano kati yao na mawaziri mbalimbali waliokuwa wakisiliza kero na changamoto zao.

Chama cha Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA), Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wajasiriamali wadogo ndio waliowasilisha kero hizo katika mkutano huo uliofanyika mjini Songea mkoani Ruvuma.

Mawaziri walioshiriki mkutano huo ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki; naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Musa Sima; naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angela Mabula na naibu Waziri wa Fedha, Dk Ashatu Kijaji.

Katibu  wa jumuiya ya wafanyabiashara mkoani Ruvuma, Wilson  Nziku amesema ubovu wa miundombinu inayounganisha Mkoa huo na nchi jirani ya Msumbiji na Malawi, utitiri wa kodi, ucheleweshaji wa malipo na Serikali kutosimamia vyema sekta ya kilimo  hasa usambazaji wa pembejeo na usimamizi wa mifumo ya masoko ya mazao ni kati ya kero hizo.

Alizitaja kero nyingine kuwa ni wakulima kutozwa ushuru kabla ya mazao kufika sokoni na kampuni kubwa kutokuwa na mfumo mzuri wa usambazaji wa pembejeo kwa kutofautisha bei ya jumla na rejareja.

Pia Soma

Advertisement
“Pia kuna mazingira magumu ya taratibu za uwekezaji hasa katika upatikanaji wa baadhi ya vibali kama vya NEMC (Baraza la Taifa la Usimamizi wa Mazingira), gharama kubwa za huduma za maji safi  na maji taka  sambamba na gharama za nishati  za umeme.”

“Pia gharama kubwa ya maeneo ya biashara  yanayomilikiwa na manispaa  mfano miji mingine vibanda vya biashara  vinavyokodishwa kwa 150,000 kwa mwezi  Ruvuma  ni kati ya Sh250,000 hadi 400,000 kwa mwezi,” amesema Nziku.

Nziku amezitaja baadhi ya kodi zikiwemo za zuio katika maeneo ya biashara, zimamoto, mabango ya biashara kuwa vikwazo, “Yaani unapaswa kuwa na leseni zaidi ya moja katika duka eti kwa kuwa  unauza  bidhaa mchanganyiko.”

Mwakilishi wa sekta ya  viwanda,  Alex Tweve  amezitaja changamoto kadhaa za biashara ikiwemo Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutoza kodi kubwa na riba pamoja na mamlaka mbalimbali za kutoa vibali vya biashara kutokuwa na ofisi mkoani humo.

Tweve amezitaja taasisi hizo ambazo hazina ofisi kuwa ni Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (Osha), NEMC na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA).

Akijibu baadhi ya kero,  Dk Kijaji alisema katika bajeti ya 2018/19 na 2019/20, Serikali ilitenga Sh600 bilioni kwa ajili ya kulipa madeni ya wazabuni na watumishi na mkoa huo ulipewa Sh500 milioni.

Mbali na kuwataka wafanyabiashara kuwa waaminifu kwa kulipa kodi, Dk Kijaji amesema Serikali imefuta tozo 54 zilizokuwa kero kwa wafanyabiashara na wawekezaji, bado inaendelea kuziondoa na kuzifanyia marekebisho ili kuweka mazingira sawa ya biashara.

Kwa upande wake Kairuki amesema Serikali imedhamiria kukuza mchango wa viwanda hasa vya mazao ya kilimo jambo litakalokuza ajira kwa  wananchi wa vijijini.

Chanzo: mwananchi.co.tz