Geita. Wachimbaji wadogo wawili wanaochimba katika mgodi wa Nyakafuru wilayani mbogwe wamepoteza maisha huku wengine wawili waliokua mgodi wa Imalanguzu wilayani Geita wakihofiwa kupoteza maisha baada ya kufukiwa na kifusi cha udongo jana oktoba mosi
Mhandisi wa migodi kutoka ofisi ya madini mkoani Geita Joseph Ng'itu amesema vifo vya wachimbaji wadogo wawili vilivyotokea kwenye machimbo ya Nyakafuru walifikwa na mauti baada mmoja kuanguka wakati akipanda kutoka kwenye shimo na kumuangukia mwingine aliyekua chini na wote kupoteza maisha.
Akizungumzia wachimbaji waliofukiwa na kifusi kwa zaidi ya saa 29 sasa eneo la Imalanguzu kata ya Lwamgasa wilayani Geita Ng'itu amesema bado wanaendelea na juhudi za kuwaokoa.
Amesema zoezi la uokozi linafanywa na wachimbaji wadogo wakishirikiana na kikosi cha uokozi kutoka jeshi la zimamoto ambapo bado wanaendelea kutoa udongo ndani ya shimo kutokana na wachimbaji hao kuwa umbali wa mita 80 chini ya ardhi.
Amesema ajali hiyo imesababishwa na matimba (magogo) wanayo tumia kuzuia udongo kuzidiwa nguvu na kuanguka.
Ng'itu amesema kwa sasa mtambo (escaveta) kutoka kampuni ya madini ya dhahabu Geita (GGM) imefika na inasaidia kuondoa udongo ili kuokoa wachimbaji hao ambao bado wako chini ya ardhi.
Pia Soma
- Kizimbani Dar kwa madai ya kusafirisha dawa za kulevya
- Moshi yafanya vizuri matumizi ruzuku ya elimu
- Fao, Serikali ya Tanzania zaja na mwongozo wa uwajibikaji katika ardhi