Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Waandishi wa habari watakiwa kujiunga na mifuko ya hifadhi za jamii

69064 Pic+waandishi

Wed, 31 Jul 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Mwanza. Rais wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Deogratius Nsokolo amewataka waandishi wa habari nchini kujiunga na mifuko ya hifadhi za  jamii kujiandalia mazingira bora ya maisha ya uzeeni.

Akifungua mkutano wa pili wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) na marafiki jijini Mwanza leo Jumatano Julai 31, 2019, Nsokolo amesema wengi wa waandishi wa habari nchini hawajajiunga na mifuko ya jamii kutokana na sababu kadhaa ikiwemo kukosa mikataba ya ajira.

"Waandishi wa habari ni hodari kuripoti taarifa za watu kukosa mafao. Lakini wengi wetu hatujajiunga kwenye mifuko hiyo. Tubadilike sasa tukikumbuka usemi wa fainali uzeeni," amesema Nsokolo

Ametoa mifano ya baadhi ya Waandishi nguli wa habari waliostaafu ambao maisha yao ya sasa hayaakisi uhodari na mchango wao kwa jamii wakati wa utumishi wao kutokana na kukosa mafao.

Awali, Mwenyekiti wa Mwanza Press Club (MPC), Edwin Soko amewataka wanachama wa klabu hiyo kujiunga kwenye mifuko ya jamii kujiandalia mafao wakati wa uzeeni.

"MPC tutashirikiana na NSSF siyo tu kuhamasisha watu kujiunga, bali pia wanachama wetu kujiunga na kunufaika na mafao mbalimbali ikiwemo ya elimu na uzazi," amesema Soko

Pia Soma

Meneja wa NSSF Mkoa wa Mwanza, Emmanuel Kahensa amewakaribisha waandishi wa Habari kujiunga na mfuko huo bila kujali kama wana mikataba wala ajira za kudumu.

"Mfumo mpya wa mifuko ya jamii inaruhusu kila mtu kujiunga na kunufaika na mafao bila kujali kama ni mwajiriwa. Hata wajasiriamali wakiwemo mama lishe, waendesha bodaboda na  wamachinga wanaweza kujiunga kupitia mfumo maalum," amesema Kahensa

Ametaja baadhi ya mafao ya muda mfupi inayotolewa na mfuko huo kuwa ni uzazi, msaada wa mazishi, matibabu na kukosa ajira kwa walioachishwa kazi.

Mkutano huo unahudhuriwa na waandishi wa habari zaidi ya 50.

Chanzo: mwananchi.co.tz