Dodoma. Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge ametoa maagizo manane kwa viongozi mkoani hapa akisema sasa watapimwa kutokana na makusanyo yatakayopatikana katika maeneo yao.
Dk Mahenge ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Agosti 3, 2018 zikiwa zimepita siku mbili tangu Rais John Magufuli kusema mkoa huo unaongoza kwa mapato kati ya majiji sita yaliyopo nchini.
Akizungumza katika hafla ya kuapishwa mkuu wa wilaya ya Dodoma Mjini, Patrobas Katambi na mkuu wa wilaya ya Bahi, Mwanahamisi Mukunda, Dk Mahenge amesema viongozi hao wanatakiwa kuhakikisha mapato yanaongezeka katika halmashauri zao.
“Pamoja na kusimamia mapato mnatakiwa kuibua vyanzo vingine vya mapato ili muongeze mapato katika halmashauri zenu na kuweza kuwaletea wananchi maendeleo,” amesema Dk Mahenge.
Maagizo mengine aliyoyatoa kwa viongozi hao ni kuzingatia muda, kusimamia vyema ulinzi na usalama, kutatua kero za wananchi, uwezeshaji wa vijana, kusimamia elimu, kujenga ushirikiano miongoni mwa viongozi na wananchi pamoja na kusimamia miradi ya maendeleo.