Musoma. Kiongozi wa mbio za Mwenge Kitaifa Mzee Mkongea amewataka vijana kuacha kulalamika kuhusu ukosefu wa ajira, badala yake watumie fursa zilizopo kujiajiri ikiwamo asilimia 10 ya mikopo ya Halmashauri inayotolewa kwa ajili yao.
Mkongea amesema kumekuwepo na tabia kwa baadhi ya vijana kushinda vijiweni kwa madai ya kukosa ajira huku wengine wakitumbukia katika matumizi ya madawa ya kulevya hivyo kuwataka kuacha mara moja, badala yake kutumia fedha hizo kwa ujasiriamali.
Akizungumza katika Kijiji cha Kurwaki, Halmashauri ya wilaya ya Musoma vijijini leo Mei 31, 2019 wakati alipotembelea kikundi cha vijana kilichonufaika na mikopo ya Halmashauri, amesema Serikali haiwezi kuajiri watu wote kwa wakati mmoja.
Amesema kwa kulitambua hilo ndio maana imeamua kutenga kiasi cha asilimia 10 ya mapato ya halmashauri kwa ajili ya mikopo ya vijana, hivyo wakiitumia vizuri itawasaidia kujiajiri na kuajiri wengine.
Kwa upande wa kijana Mjenga Nyamarwa amesema kuwa umefika muda sasa vijana wajiunge katika vikundi ili iwe rahisi kupatiwa mikopo kwa ajili ya kuanzisha shughuli za uzalishaji.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya hiyo John Kayombo amesema kuwa hadi sasa Halmashauri yake imekwishatoa asilimia 96 ya mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.
Pia Soma
- Wiki ya elimu inasaidia kuongeza ufaulu katika maeneo inakoadhimishwa
- VIDEO: Serikali yamkana Hapi kuhusu vitambulisho
- VIDEO: Wanaume wakware wapewa dawa ya kutowatamani wanafunzi wa kike
Mwenge wa Uhuru uko katika halmashauri ya Wilaya ya Musoma vijijini na unatarajiwa kukakua, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi sita yenye thamani ya zaidi ya Sh3 bilioni.