Idadi ya watu waliokufa kutokana na ajali ya basi kugonga lori mkoani Singida imefikia tisa na wanane ni majeruhi.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Pipi Kayumba alisema basi hilo, Ludigija Express lilikuwa likitoka Dar es Salaam kwenda Mwanza.
Alisema ajali hiyo ilitokea jana saa 11 alfajiri katika Kijiji cha Malendi mpakani mwa Wilaya ya Iramba na Igunga kwenye barabara kuu ya Singida - Mwanza.
Kamanda Kayumba alisema basi hilo lenye namba za usajili T 315 CXX liligonga kwa nyuma lori la mizigo lililokuwa limeharibika na kuegeshwa kando ya barabara hiyo.
Alisema dereva wa basi hilo alikimbia baada ya ajali na anatafutwa na akabainisha kuwa watu saba walikufa kwenye eneo la ajali.
Alitaja lori lililogongwa kuwa ni aina ya DAF lenye namba za usajili T 485 DBR likiwa na tela lenye namba za usajili T 235 DSE lililokuwa likiendeshwa na Mohamed Ali (54) mkazi wa Dar es Salaam.
Kamanda Kayumba alisema wakati wa ajali mvua ilikuwa ikinyesha na kulikuwa na ukungu mwingi lakini dereva wa basi hakuchukua tahadhari hivyo kusababisha ajali hiyo.