Ukerewe. Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella amelazimika kutumia mwanga wa taa za nguvu ya jua pamoja na tochi za simu kuzungumza na wakazi wa kisiwa cha Siza wilayani Ukerewe kulikotokea mauaji ya watu wanne akiwemo ofisa mfawidhi wa rasilimali za uvuvi kanda ya Ukerewe, Ibrahim Nyaghali.
Akiwa ameambatana na viongozi wengine wakiwemo wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa huo, Mongella aliyefika kisiwani humo jana usiku Jumanne Julai 23, 2019 aliwataka wananchi kuwa watulivu na kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha uvunjifu wa amani na utulivu.
Akizungumza na wananchi hao saa 2 usiku muda mfupi baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Mkuu wa wilaya ya Ukerewe, Cornel Maghembe na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro.
Mongella amesema tukio hilo limetia doa siyo tu wilaya ya Ukerewe na mkoa wa Mwanza, bali Taifa kwa ujumla na halistahili kujirudia tena.
"Tutahakikisha haki inatendeka ili watu waliohusika na kitendo hiki waweze kuchukuliwa hatua," amesema Mongella
Tukio hilo lilitokea Julai 22, 2019 katika kisiwa cha Siza kata ya Ilagangala wakati ofisa huyo aliyeambatana na askari alipokwenda kukamata wanaotumia nyavu haramu.