Iringa. Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Ally Hapi amewashukia baadhi ya viongozi wastaafu walioamua kumhujumu Rais wa Tanzania John Magufuli.
Hapi amesema hayo leo Julai 21 ofisini kwake wakati akizungumza na wanahabari kuhusu kuibuka kwa mijadala mbalimbali ndani ya nchi inayoigusa Serikali inayoongozwa Magufuli.
Hapi amesema mijadala hiyo imewahusisha baadhi ya viongozi hao wastaafu waliotumikia nchi kwa kipindi kirefu.
“Jitihada za wastaafu hao zimelenga kupeleka mashambulizi kwa Rais wetu, lakini zikiwa na maana ya kuligawa Taifa letu; ni mambo ambayo sote tumeyashuhudia siku za hivi karibuni,” amesema.
“Na mimi kama mkuu wa mkoa niliyeteuliwa na Rais Magufuli niliyekula kiapo kutetea katiba na kulinda umoja na mshikamano wa nchi siwezi kukaa kimya.
“Mimi kama mkuu wa mkoa niliyelelewa kwenye chama na bahati mbaya au nzuri wazee hawa ambao wamekuwa wakitoa nyaraka na matamko mbalimbali ni wazee ambao tumekuwa kwenye chama tukiwaheshimu sana kama viongozi wetu ndani ya chama,”amesema.