Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila ametangaza kuendelea kwa Operesheni kali ya kudhibiti upitishwaji holela wa bidhaa mbalimbali za magendo katika fukwe za bahari ya Hindi ambapo amesema yoyote atakaye kamatwa adhabu kali itachukuliwa dhidi yake kwa mujibu wa sheria za nchi.
RC Chalamila amebainisha bidhaa za magendo zilizokamatwa ni mifuko ya sukari zaidi ya 100, madumu ya mafuta ya kupikia zaidi ya 700 pamoja watuhumiwa zaidi ya 7 ambapo ameagiza watuhumiwa wote wachukuliwe hatua kali za kisheria.
Aidha RC Chalamila amesema bidhaa hizo zilizokamatwa zimetoka upande wa Zanzibar kuja Tanzania bara kwa kutumia mashua "Kushamiri kwa uingizaji wa bidhaa za magendo ni kulikosesha Taifa mapato lakini pia ni hatari kwa afya za binadamu kwa kuwa bidhaa hizo zinakuwa hazija pimwa ubora" amesisitiza RC Chalamila.
Ifahamike kuwa bidhaa hizo za magendo zimekamatwa usiku wa kuamkia jana Februari 10 kupitia kikosi kazi cha kudhibiti mtandao mzima wa upitishwaji wa bidhaa za magendo katika fukwe za bahari ya Hindi.