Dar es Salaam. Muda mfupi baada ya Rais wa Tanzania, John Magufuli kumteua Julius Mtatiro kuwa mkuu wa Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma kumekuwa na maoni tofauti katika mitandao ya kijamii kuhusu uteuzi huo.
Katika maoni hayo hasa katika mtandao wa kijamii wa Twitter, wengi wamehusisha uteuzi huo na uamuzi wa Mtatiro kuhamia CCM akitokea CUF alikokuwa naibu katibu mkuu wa chama hicho.
Mtatiro aliyechukua nafasi ya Juma Homera aliyeteuliwa kuwa mkuu wa Mkoa wa Katavi alihamia CCM Agosti, 2018.
Wakitoa maoni katika ukurasa wa mkurugenzi wa mawasiliano ya Rais, Ikulu Gerson Msigwa, Gaima Tz @GaimaTz amempongeza Mtatiro, lakini akahoji kuhusu wapinzani wanaohamia CCM na kupewa vyeo.
“Hongera Julius Mtatiro na mwana-UDSM mwenzangu kwa uteuzi huo japokuwa tuwe wazi na kweli kuwa tuelewe mbegu tunayopanda kwa makada wa CCM waliokipigania chama hadi kupata ushindi wa kuunda serikali, sasa imegeuka kuwa wahamiaji ndiyo bora kuliko waliokipambania na makada wa CCM,” amesema Gaima Tz @GaimaTz.
Mchangiaji mwingine, @MakuruRobert amesema,“Hongera kwa kuteuliwa ili ukazuie mikutano ya wapinzani marafiki ulioachana nao katikati ya vita ya uhuru wa kutoa maoni, kuvumiliana na kuwa na siasa za kistaarabu. Hayo ndio uliyategemea haswa siku uliposema wewe bado kijana na una familia inakutegemea.”
Pia Soma
- Mfanyabiashara maarufu wa Tanzania aliyeuawa na al-Shabab azikwa Somalia
- Ufaransa yaahidi kushirikiana na Magufuli
- BoT yamuondoa Nyabundege TIB Corporate
Maoni hayo yameungwa mkono na Ibrahim R Nyanza akisema anaamini utendaji wa Mtatiro.
“Hii safi sana. Naamini utendaji wa ndugu Mtatiro, naamini hatomuangusha Rais katika utekelezaji wa ahadi mbalimbali za Chama cha Mapinduzi kwa wana Tunduru,” amesema Nyanza.