Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Upendo wa vijana kubeba jeneza Dar waibua sintofahamu

94741 Msiba+pic Upendo wa vijana kubeba jeneza Dar waibua sintofahamu

Thu, 6 Feb 2020 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Alikuwa rafiki wa kweli. Ndivyo unavyoweza kusema ukiwazungumzia baadhi ya wakazi wa mtaa wa Tabata Kisiwani jijini Dar es Salaam  waliobeba jeneza la  Emmanuel Cosmas  umbali wa zaidi ya mita 800 kabla ya kulipakia kwenye gari kwenda Kilosa, Morogoro kwa mazishi.

Wamesema wameamua kumsindikiza rafiki yao kwa miguu kutoka kanisani hadi eneo la Tabata Relini maarufu Tabata Mwananchi ambako kulikuwa na magari yanayokwenda Morogoro.

Kitendo hicho kilizua sintofahamu kwa kuwa baadhi ya watu waliopisha nao walidhani kuna mgogoro wa kifamilia.

Wakizungumza na Mwananchi, wakazi wa mtaa huo wamesema walimpenda mwenzao kwa sababu alikuwa mnyenyekevu na alipenda zaidi kusaidia watu.

 “Emmanuel alikuwa kama familia, nyumbani kwangu ilikuwa kama kwake. Alikuwa akitusaidia mimi na wapangaji wenzangu kazi ndogondogo kwa malipo ambayo hakuwahi kupanga, aliridhika na kiasi chochote,” amesema mkazi wa mtaa huo, Alex Malanga.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Tabata Kisiwani, Rajabu Chala amesema hakukuwa na tatizo lolote bali vijana wenzake wametaka kumbeba rafiki yao kipenzi ambaye waliishi naye vizuri. Amesema alifariki dunia Februari 4, 2020.

Pia Soma

Advertisement
“Anasafirishwa kwenda Kilosa kwa ajili ya mazishi na vijana wamechangisha fedha kwa ajili ya usafiri. Safari hii inaanzia hapa Tabata Mwananchi kuelekea huko,” amesema mwenyekiti huyo.

Japhet Kanyika, rafiki wa karibu wa marehemu amesema alikuwa akisumbuliwa na ngiri kwa muda mrefu na alifanyiwa upasuaji.

“Hapa Dar es Salaam hakuwa na ndugu yoyote, amekuwa akiishi mwenyewe. Anapendwa sana na watu ndiyo maana unaona umati huu wote wamekuja hapa kumuaga,” amesema kijana huyo.

Kijana mwingine, Ramadhan Adam amesema marehemu alikuwa akifahamika kama “Rais” kwa sababu ni mtu wa watu, anapendwa na watu wote, watoto kwa wakubwa. Amesema hajawahi kusikia amepigana na mtu.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz