Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abubakar Kunenge amesema kuwa matarajio ya mkoa huo kwenye suala la upatikanaji wa maji ni kufikia 100% ifikapo mwaka 2024 ambapo hadi sasa 92% tayari zimeshakamilika.
Kunenge amebinisha hayo kwenye sherehe ya kuzindua Daraja la Juu la Kijazi Jijini Dar es Salaam ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Rais Dk John Pombe Magufuli.
“Haya ni mafanikio makubwa sana muheshimiwa Rais kwasababu ilani yetu ya chama imeelekeza mkoa huu ufikie upatikanaji wa maji safi na salama kwa asilimia 95 itakapofika mwaka 2025 tunakupongeza kufikia rekodi kubwa ya kuingia uchumi wa kati kabla ya wakati na sasa umeweka rekodi nyingine kufikisha 100% za upatikanaji wa maji mkoani humu kabla ya muda” amesema Kunenge.
Aidha Kunenge amesema kuwa kupitia uongozi mzuri wa Dk Magufuli mkoa huo umepata kiasi cha fedha takribani trilioni 1.93 kwa ajili ya miradi ya ujenzi wa barabara kitu kilichopelekea kuwepo wa barabara za lami kilometa 279 iliyotekelezwa na Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) pamoja na Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA).