WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) Ummy Mwalimu amemsimamisha kazi Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Sengerema, Magesa Boniphase kuanzia jana ili kupisha uchunguzi dhidi yake.
Hayo yalisemwa jana na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano katika Ofisi ya Tamisemi Serikalini, Nteghenjwa Hosseah.
Alisema Ummy amechukua hatua hiyo baada ya kupokea malalamiko na tuhuma za ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema kutoka kwa wananchi na viongozi, akiwemo Mbunge wa Sengerema, Hamisi Tabasamu.
Alisema tuhuma hizo zumeelekezwa kwa Mkurugenzi Mtendaji na baadhi ya wakuu wa idara za halmashauri hiyo na zinaonesha kuwa, mkurugenzi huyo kwa kushirikiana na wakuu hao wa idara wamefanya ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Alisema fedha hizo zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo katika halmashauri hiyo hivyo kuathiri utekelezaji wa miradi kwa kiwango kilichokusudiwa.
“Kutokana na tuhuma hizo, Waziri Ummy amemuagiza Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Tamisemi kuunda tume ya uchunguzi wa tuhuma hizo haraka,” alisema.
Aidha, Hosseah alisema Waziri Ummy pia amemuelekeza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza kuhakikisha katika kipindi chote ambacho tume hiyo ya uchunguzi ikifanyakazi katika halmashauri hiyo malipo yote yatakayofanyika kuanzia sasa yazingatie sheria, kanuni na taratibu za usimamizi wa fedha za umma.