Musoma. Wakati tathmini kuhusu athari ya mvua iliyonyesha jana wilayani Musoma Mkoa wa Mara na kusababisha kifo cha mtu mmoja, wakazi katika maeneo yaliyokumbwa na mafuriko wamesema chanzo ni ujenzi holela.
Wakizungumza leo Jumapili Desemba Mosi, 2019 baadhi ya wakazi hao wamesema mafuriko yametokana na watu kujenga kwenye mkondo ya maji na kusababisha yakose mwelekeo mvua inapokuwa kubwa.
Getruda Joash, mkazi wa Machinjioni amesema ameishi maeneo yaliyokumbwa mafuriko zaidi ya miaka 30 lakini hajawahi kuona mafuriko kama yaliyotokea jana.
Maeneo yaliyokumbwa na mafuriko ni mitaa ya Machinjioni, Kariakoo, Mshikamano, Kitaji na Nyakato.
Stella Jonathan amesema Serikali inapaswa kuingilia kati ujenzi wa nyumba katika mitaa hiyo ili kuwanusuru wananchi.
Mkuu wa wilaya ya Musoma, Dk Vicent Naano amesema bado tathmini ya maafa hayo inafanyika, na kwamba baadhi ya watu waliokosa makazi wamepewa hifadhi kwa ndugu na jamaa zao Mkuu huyo wa wilaya ameziagiza mamlaka husika kusitisha ujenzi mabondeni kuepuka maafa zaidi na kuzitaka familia zinazoishi katika maeneo hayo kuhama.